Mwenyekiti wa Taasisi ya sekta Binafsi (TPSF) Bw. Reginald Mengi wa pili kushoto akieleza jambo wakati wa kikao baina ya TPSF na Wizara.
Wanaosikiliza ni Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF Bw. Godfrey Simbeye na
(katikati mbele) ni Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Bw. Eliakim
Maswi.
Baadhi ya Wawakilishi kutoka Sekta Binafsi (TPSF) waliofika katika kikao
hicho wakifuatilia kikao hicho.
Na Asteria Muhozya,
Ujumbe kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF), umekutana na
uongozi wa Wizara ya Nishati na Madini ili kujadili masuala mbalimbali
ya namna sekta binafsi zinavyoweza kushiriki katika uchumi wa gesi na
mafuta nchini.
Ujumbe huo ulioongozwa na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo Bw. Reginald
Mengi na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Bw. Godfrey Simbeye
pamoja na wawakilishi wengine wa Taasisi hiyo ulifika wizarani jana
kukutana na uongozi wa Wizara.
Aidha, ujumbe huo ulipata nafasi ya kukutana na Katibu Mkuu Wizara ya
Nishati na Madini Bw. Eliakim Maswi na baadhi ya Watendaji wa Wizara
wanaoshughulikia masuala ya Nishati, ambapo TPSF walipata fursa ya
kuwasilisha mapendekezo yao kuhusu namna ambavyo watashiriki katika
uchumi wa gesi.
Wakiongozwa na Mwenyekiti wao, wajumbe toka TPSF walieleza nia
yao ya kushiriki katika uchumi wa gesi na kueleza mikakati ya namna
watakavyoshiriki ili sekta iweze kuwa na manufaa kwa Watanzania wote
na hivyo kuongeza pato la nchi na kufikia maendeleo tarajiwa.
Pamoja na hayo, Mwenyekiti wa sekta binafsi Bw. Reginald Mengi
alitumia fursa hiyo kueleza kuwa, kikao hicho kimefungua ukurasa mpya
wa ushirikiano ili nchi iweze kuweza kufikia kule Watanzania na Taifa
linakotarajia kufika.
“Naondoka katika kikao hiki nikiwa na amani sana. Yaliyopita yamepita
na yamekwisha. Tunataka kufanya kazi pamoja na Wizara katika sekta ya
gesi. Tumekuja hapa kama Watanzania, tujue tutafanya kazi namna gani
katika sekta hii”. Alisema Mengi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara hiyo Bw. Eliakim Maswi,
aliushukuru ujumbe huo kwa kufika katika mazungumzo hayo na kueleza
kuwa, nia ya Wizara na Serikali ni kuona Watanzania wote wanashiriki
katika uchumi huo. Aidha, aliongeza kuwa, Wizara inayachukua
mapendekezo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi.
“Kwetu sisi tunataka kuona watanzania wanashiriki katika uchumi huu.
Tuko tayari kufanya kazi na ninyi. Tufungue milango, tusaidiane huku
tukiendeleza utulivu na uvumilivu. Mimi na wataalam wangu tutayafanyia
kazi”. Alisema Maswi.
TPSF keep persisting! Future generation will Honor you.
ReplyDelete