Sign in to confirm you’re not a bot
This helps protect our community. Learn more
UJERUMANI YAAHIDI KUSAIDIA UKRAINE KUTENGENEZA MAKOMBORA YA MASAFA MAREFU
5Likes
555Views
May 292025
Berlin. Kansela mpya wa Ujerumani, Friedrich Merz, ameahidi kuiimarisha Ukraine kwa kuiwezesha kutengeneza makombora ya masafa marefu, katika jitihada za kujilinda dhidi ya mashambulizi ya Urusi. Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jijini Berlin akiwa na Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, Merz alisema kuwa mazungumzo ya uzalishaji wa makombora hayo yanaendelea, lakini hakufichua maelezo ya kina kuhusu aina ya silaha zitakazohusika. Alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kuipatia Ukraine makombora ya Taurus, alijibu kwa tahadhari, akisema: "Tunataka kuzungumzia kuhusu uzalishaji, lakini hatutajadili kwa hadhara maelezo ya kina." Makombora ya Taurus yana uwezo wa kufika hadi umbali wa kilomita 500 (sawa na maili 310), na hivyo yanaweza kufika ndani kabisa ya eneo la Russia, jambo linalozua wasiwasi wa kimataifa kuhusu kusambaa kwa vita. Ingawa Kansela Merz hakulitaja moja kwa moja jina la kombora hilo, alibainisha kuwa “makubaliano ya awali” kuhusu uzalishaji wa makombora hayo yatasainiwa baadaye Jumatano na mawaziri wa ulinzi wa Ujerumani na Ukraine. Merz, aliyeingia madarakani mapema mwezi huu, ameashiria mabadiliko ya msimamo wa Ujerumani kuhusu silaha, akisema kuwa hakutakuwa tena na vikwazo kuhusu masafa ya silaha zinazotolewa kwa Ukraine kutoka kwa mataifa ya Magharibi. Hili linachukuliwa kama hatua mpya ya ujasiri katika sera za Ujerumani kuhusu mzozo wa Ukraine. Moscow imetoa onyo kali dhidi ya hatua yoyote ya kuondoa vikwazo vya silaha kwa Ukraine, ikisema kuwa hiyo ni "mabadiliko hatari ya sera" na inaweza kuathiri juhudi za kufanikisha makubaliano ya kisiasa. Hata hivyo, Merz amesema kuwa uamuzi huo wa kuondoa mipaka ya masafa ya silaha ulifikiwa kwa pamoja na washirika wa Magharibi miezi kadhaa iliyopita. Kwa upande wake, Zelensky amependekeza kufanyika kwa mkutano wa amani unaowahusisha yeye mwenyewe, Rais wa Russia Vladimir Putin, na Rais wa Marekani Donald Trump. Ingawa msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov hakupinga wazo hilo moja kwa moja, alisema kuwa mkutano wa aina hiyo unaweza tu kufanyika baada ya wajumbe wa pande hizo mbili kufikia makubaliano ya msingi. Mazungumzo ya kwanza ya moja kwa moja kati ya Ukraine na Russia tangu kuanza kwa vita yalifanyika mjini Istanbul mwezi huu, yakihusisha maofisa wa ngazi ya chini. Makubaliano pekee yaliyofikiwa yalihusu kubadilishana wafungwa, ambayo yalitekelezwa mwishoni mwa wiki iliyopita. Katika hatua nyingine, Rais wa Marekani Donald Trump ameonyesha kufadhaika na kusuasua kwa mazungumzo ya amani. Amesema kuwa uvumilivu wake na Russia umefikia kikomo, akiilaumu Moscow kwa kuchelewesha mazungumzo huku ikizidisha mashambulizi. Trump alitoa matamshi hayo baada ya kombora la Russia kuua raia 13 nchini Ukraine, wakiwemo watoto. Russia ilijibu kwa kusema kuwa Trump hana taarifa kamili kuhusu muktadha wa kijeshi wa tukio hilo. Zelensky ameisihi Marekani kuiwekea Russia vikwazo vya ziada katika sekta ya benki na nishati, akisema kuwa tayari amezungumza na Trump kuhusu hilo. Trump, kwa upande wake, alithibitisha kuwa vikwazo hivyo vitawekwa endapo Russia haitaacha mashambulizi. Jeshi la Ukraine limeripoti shambulio kubwa la droni dhidi ya malengo ya Russia, huku Zelensky akieleza kuwa zaidi ya droni 900 za Russia zilirushwa ndani ya siku tatu tu hadi Jumatatu. Kwa upande mwingine, Moscow inaripotiwa kuwa inakusanya wanajeshi zaidi ya 50,000 katika eneo la Sumy, kaskazini mashariki mwa Ukraine. Gavana wa Sumy, Oleh Hryhorov, amesema kuwa vijiji vinne tayari vimechukuliwa na vikosi vya Russia, na mapigano yanaendelea katika maeneo ya jirani. Vita kati ya Ukraine na Russia sasa vinaingia mwaka wa nne, vikiwa tayari vimesababisha vifo vya makumi ya maelfu ya watu na kuharibu sehemu kubwa ya mashariki na kusini mwa Ukraine. Russia bado inashikilia takribani asilimia 20 ya ardhi ya Ukraine, ikiwemo Crimea, ambayo ilitwaa mwaka 2014. Zelensky ameishutumu Moscow kwa kuvuruga juhudi za amani kwa kushindwa kuwasilisha waraka wa masharti ya amani kama walivyoahidi baada ya mazungumzo ya Istanbul. Peskov amesema kuwa waraka huo uko katika "hatua za mwisho za maandalizi." IMEANDALIWA NA HELLEN MDINDA, KWA MSAADA WA MASHIRIKA YA HABARI

Mwananchi Digital

1.15M subscribers