JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA
YA NISHATI NA MADINI
TAARIFA
YA UFAFANUZI KUHUSU KIKAO CHA WAZIRI WA NISHATI NA MADINI MHE. PROF. SOSPETER
MUHONGO (MB.) NA UJUMBE WA BENKI YA DUNIA KILICHOFANYIKA TAREHE 28.09.2016
Wizara ya Nishati na Madini inapenda
kutoa ufafanuzi kuhusu kikao cha Waziri wa Nishati na Madini na Ujumbe wa Benki
ya Dunia kilichofanyika tarehe 28.09.2016 kikihusishwa na kupandishwa kwa bei
ya umeme kama ilivyoripotiwa na magazeti ya Mwananchi ya tarehe 12.01.2017
lenye kichwa cha habari “Prof. Muhongo alivyoshiriki kupandisha bei
ya umeme” na la tarehe 13.01.2017 lenye kichwa cha habari “Prof.
Muhongo awekwa mtu kati”.
Wizara inapenda kuutaarifu Umma kuwa,
imekuwa ikifanya vikao na wadau mbalimbali wakiwemo Taasisi za Umma, Binafsi na
Washirika wa Maendeleo yakiwemo Mashirika ya Kifedha ya Kimataifa. Lengo la
vikao hivyo ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika Sekta za Nishati na
Madini nchini.
Aidha, tarehe 28/9/2016 Wizara
ilifanya kikao na Ujumbe kutoka Benki ya Dunia ikiwa ni mwendelezo wa vikao vya
majadiliano kuhusu upatikanaji wa mkopo wa Dola za Marekani Milioni 200 kwa
ajili ya kuboresha uendeshaji wa Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO). Kikao
hicho pia kilihudhuriwa na taasisi nyingine zikiwemo Wakala wa Nishati Vijijini
(REA), Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Shirika la Maendeleo la Petroli
Tanzania (TPDC), Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC) na Mamlaka ya Udhibiti wa
Nishati na Maji (EWURA).
Katika kikao hicho masuala
yaliyojadiliwa yalikuwa ni;
1. Upatikanaji wa
umeme wa kutosha, uhakika na bei nafuu kwa
ajili ya kuchochea shughuli za maendeleo ya kukuza uchumi wa nchi ikiwemo
viwanda, biashara, kilimo na huduma za jamii;
2. Kuongeza ufanisi wa
utendaji wa Shirika la Umeme (TANESCO); na
3. Kupunguza deni la
TANESCO.
Katika kulipunguza deni la TANESCO
ambalo linakaribia Shilingi Bilioni 800
(takriban Dola za Marekani Milioni 363) na kuboresha shughuli za utendaji
za TANESCO, Benki ya Dunia ilijadiliana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara
ya Nishati na Madini ili kupata mkopo wa Dola
za Marekani Milioni 200. Hivyo, katika kikao hicho, hakukuwa na makubaliano
ya kupandisha bei ya Umeme kama ilivyoripotiwa na gazeti hilo.
Vile vile, tunaomba kuutaarifu Umma
kwamba Wizara ya Nishati na Madini kwa niaba ya Serikali inafanya majadiliano
na Benki ya Maendeleo ya Africa (AfDB), Umoja wa Ulaya (EU), JICA (Japan), na
Mashirika mengine ya fedha kwa lengo la kutafuta fedha za kuboresha Sekta ya
Nishati.
Imetolewa na;
WIZARA YA NISHATI NA MADINI
13.01.2017
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...