Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Askari wa Wanyamapori wa Pori la Akiba la Selous, Kanda ya Kaskazini Mashariki Kingupira imewaokoa wafugaji 50 waliokuwa wakiwapitisha jumla ya ng’ombe 1780, kondoo 200 na punda 6 baada ya kutelekezwa kwa muda wa siku tano na mtu mmoja aliyetajwa kwa jina la Mzigua aliyewarubuni kwa kuwaonyesha njia za mkato ndani ya Pori hilo wao bila kujua na kuamua kuwakimbia. 

Bw. Lisasi Cherehani ambaye ni mmoja wa wafugaji hao alisema ‘’tulimpa Mzigua kiasi cha zaidi ya shilingi 5,000,000 kutoka kwa wafugaji kama malipo ya kutufikisha eneo la Ilonga mkoani Morogoro tukitokea vijiji vya Ndundunyekanza, Kipungila na Chumbi vilivyopo wilayani Rufiji mkoani Pwani kwa makubaliano kuwa atatupitisha njia fupi ya mkato tutakayotembea kwa muda wa siku tano tu, hatukujua anatutupitisha ndani ya pori hili. ‘’

Baada ya kutelekezwa, wafugaji hao ambao walikuwa katika hali mbaya waliomba msaada kwa ndugu zao ambao waliwasiliana na Uongozi wa Pori la Akiba la Selous ambao kwa haraka walifanya jitihada za kuokoa maisha yao ikiwa ni kuwapa huduma ya kwanza, maji, uji pamoja na kuwakimbiza hospitalini kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence Milanzi aliwatembelea wafugaji hao jana kwa ajili ya kuwapa pole na kuwapelekea chakula yakiwemo maji pamoja na unga.

Aidha, Milanzi aliagiza Wafugaji hao waachiwe huku akitoa wito kwa wananchi kuacha kupita maeneo ya Hifadhi kwa vile ni kosa kisheria na wale wote watakaobainika watachukuliwa hatua za kisheria na kuahidi kuwa mtu huyo aliyewa danganya kwa kuwapitisha ndani ya Hifadhi hiyo ni lazima akamatwe kwa udi na uvumba.

‘’Sisi kama Serikali kitu cha kwanza ni ubinadamu tumewahudumia na hivyo natoa tamko la kuwaachia wafugaji wote waliopotea ndani ya Pori hili kwa vile mateso waliyoyapata na mali waliyoipoteza ni kubwa sana baada ya kudanganywa kwa na kupitishwa ndani ya Pori la Akiba la Selous.’’ Alisema Milanzi
   Baadhi wa Wafugaji wakiwa wanakunywa maji na juisi walizopelekewa kama msaada baada ya kuokolewa na Askari wanyamapori wa Pori la Akiba la Selous,  Kanda ya Kaskazini Mashariki  Kingupira  baada ya kutelekezwa kwa muda wa  siku tano na mtu mmoja waliyemtaja kwa  jina maarufu la Mzigua aliyewarubuni kwa kuwaonyesha njia za mkato ndani ya Pori hilo ( Picha na Lusungu Helela-Wizara ya Maliasili na Utalii) 
  Baadhi ya Mzoga wa ngombe uliopatikana ndani ya Pori la Akiba la Selous,  Kanda ya Kaskazini Mashariki  Kingupira  baada ya Wafugaji 50  waliotelekezwa kwa muda wa  siku tano na mtu mmoja waliyemtaja kwa  jina maarufu la Mzigua aliyewarubuni kwa kuwaonyesha njia za mkato ndani ya Pori hilo na kisha kuwakimbia( Picha na Lusungu Helela-Wizara ya Maliasili na Utalii)
   Mmoja wa  wafugaji aliyepotea na  kutelekezwa ndani ya Pori la Akiba la Selous,  Bw. Lisesi Cherehani aliyekuwa na ng’ombe 180 na punda mmoja akiangalia mmoja wa ng'ombe wake aliyekufa kwa kukosa  maji ya kunywa kwa muda  wa siku tano kwenye Kanda ya Kaskazini Mashariki katika Pori la Akiba la Selous ( Picha na Lusungu Helela-Wizara ya Maliasili na Utalii)
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Maj. Gen. Gaudence  Milanzi (katikati) akipata taarifa kutoka kwa  Meneja wa Mradi wa Pori la Akiba la Selous    Bw. Enock Msocha (wa tatu kushoto)  mara baada ya  kuwasili kwa ajili ya kuwatembelea  Wafugaji 50 waliokolewa na Askari wanyamapori baada ya kutelekezwa  na mtu mmoja waliyemtaja kwa  jina maarufu la Mzigua aliyewarubuni kwa kuwaonyesha njia ya mkato ndani ya Pori hilo na kisha kuwakimbia ( Picha na Lusungu Helela-Wizara ya Maliasili na Utalii)

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...