Na Beatrice
Lyimo-MAELEZO
Dar es Salaam
Mfumuko wa Bei wa
Taifa kwa mwezi Novemba 2016 umeongezeka hadi kufikia asilimia 4.8 kutoka
asilimia 4.5 iliyokuwapo mwezi Octoba,
2016 kutokana na kuongezeka kwa bei ya
bidhaa na huduma katika maeneo mbalimbali nchini.
Akizungumza na
waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za
Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Bw. Ephraim Kwesigabo amesema kuwa bidhaa
za vyakula zikiwemo ngano,mbogamboga, mtama, na vinywaji baridi zimechangia kuongezeka kwa mfumuko wa bei nchini.
“Bidhaa nyingine
zilizochangia kuongezeka kwa mfumuko wa bei nchini ni Nishati , mafuta na viatu huku akibainisha kuwa kipimo
kinachotumika kupima mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zinazotumiwa na kaya
nchini zimeongeka na kufikia 104.32 kwa mwezi Novemba 2016 ikilinganishwa na 99.54
za mwezi Novemba mwaka jana” Alisema Kwesigabo.
Kwa upande wa mfumuko wa bei unaopimwa kwa kipimo cha mwezi ameeleza kuwa
umeongezeka kwa asilimia 1.1 kwa mwezi Novemba ikilinganishwa na asilimia 0.1 ya
mwezi Octoba kutokana na kuongezeka kwa Fahirisi ya baadhi ya bidhaa zikiwemo unga
wa ngano, unga wa mihogo, unga wa mahindi, mtama, dagaa, mchele.
Aidha, alisema kuwa
thamani ya shilingi ya Tanzania hupima badiliko katika kununua bidhaa na huduma
zilezile za mlaji ambazo shilingi ya Tanzania ingeweza kununua katika kipindi
tofauti, ikiwa fahirisi za bei za Taifa zinaongezeka uwezo wa shilingi ya Tanzania
katika kununua bidhaa na huduma hupungua.
Kwa upande wa mfumuko wa bei wa Tanzania na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki Kwesigabo
alisema kuwa una mwelekeo unaofanana
ambapo Kenya umeongezeka na kufikia
asilimia 6.68 mwezi Novemba kutoka 6.42 za mwezi Octoba huku Uganda ikiwa na
mfumuko wa bei wa asilimia 4.6 mwezi Novemba kutoka asilimia 4.5 za mwezi Octoba.
kurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii Epharaim Kwesigabo akiongea na wanahabari (hawapo pichani) kuhusu hali ya mfumuko wa bei kwa mwezi Novemba mwaka huu, kulia kwake ni Mtakwimu Bw. Muhidini Mtindo.
Wanahabari wakimsikiliza Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii Epharaim Kwesigabo (hayupo pichani) wakati akielezea hali ya mfumuko wa bei kwa mwezi Novemba mwaka huu. (Picha na Benjamin Sawe-Maelezo).
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...